Sunday 24 April 2016

Kauli ya First lady wa Tanzania Mama Magufuli kuhusu WAMA

MKE wa Rais John Magufuli, Janeth huenda akakwepa kuanzisha taasisi ya huduma za jamii tofauti na ilivyokuwa kwa watangulizi wake wawili, Anna Mkapa na Salma Kikwete.


Vyanzo mbalimbali vililithibitishia Nipashe kuwa ni dhahiri mke huyo wa Rais hatafanya kama walivyowahi kufanya wenzake.
“Kwa sasa hakuna dalili zozote za kuanzisha taasisi na nadhani hata mheshimiwa (Rais) mwenyewe hatapenda kuona inaanzishwa kwa hofu kwamba inaweza kupokea misaada ambayo itachafua taswira ya Ikulu mbele ya jamii,” kilisema chanzo chetu. 

“Ikianzishwa wafanyabiashara wengi watapenda kuonekana wakitoa msaada sasa watu ambao wanajijua ni wachafu wanaweza kutumia mwanya huo kutoa misaada kama njia ya kutaka huruma ama kujitakasa na mwisho wa siku taswira nzuri iliyopo inaweza kuchafuka,” kilisema zaidi chanzo chetu serikalini.

Iwapo hataanzisha taasisi kama ilivyokuwa kwa wenzake, Janeth atakuwa amefuata nyayo za mke wa Rais Ali Hassan Mwinyi na wa hayati Baba wa Taifa, Mama Maria Nyerere, ambaye kwa miaka yote 25 ambayo mume wake alikaa Ikulu kuanzisha taasisi wala kufanya biashara.

Licha ya kutoanzisha taasisi, Mama Maria hakuwahi kukumbwa na kashfa ya kujihusisha na biashara yoyote kwa muda wote mumewe alipokuwa Ikulu.
Atakuwa amejitofautisha na wenzake Anna Mkapa na Salma Kikwete ambao miezi michache tu baada ya waume zao kuingia Ikulu walianzisha taasisi kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kijamii.

Anna ambaye mume wake Benjamin Mkapa aliingia madarakani mwaka 1995-2005, muda mfupi tu baada ya kuingia Ikulu alianzisha taasisi inayoitywa Fursa Sawa kwa Wote (EOTF), ofisi zake zikiwa jirani kabisa na Ikulu.

Anna aliitumia taasisi yake kuwainua wanawake kwa kuwapa mafunzo ya ujasiriamali na wakati mwingine mikopo midogo midogo kwa ajili ya kuanzisha biashara.

Salma naye ambaye mume wake, Rais Mstaafu Jakaya Kikwete, aliingia madarakani mwaka 2005-2015, alianzisha taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA), Oktoba 2006 ikitumia ofisi zilizoachwa na EOTF.
Taasisi yake kama inavyojitambulisha ilijikita kuwasaidia wanawake, hasa wasichana kuhakikisha wanapata huduma bora za afya na elimu na ilisimamia ujenzi wa shule ya wasichana ya WAMA Nakayama iliyoko kijiji cha Nyamisati Rufijii, ambayo ilizinduliwa rasmi na Kikwete Oktoba mwaka jana.

Baadhi ya watu waliozungumza na Nipashe wamekuwa na maoni tofauti kuhusu wake za marais kuanzisha taasisi hizo wengi wakisema zinatumiwa vibaya na wafanyabiashara.

Mmoja wa watu waliohojiwa alisema taasisi hizo zinaweza kutumiwa vibaya na watu wanaotaka kujipenyeza Ikulu ili wapate upendeleo kwenye masuala mbalimbali, hasa biashara zao.
Alisema wafanyabiashara hupigana vikumbo kwenda kutoa misaada kwenye taasisi hizo za wake wa marais wanapokuwa madarakani lakini wanapotoka taasisi hizo hufilisika.

“Ushahidi wa hilo ni kwamba waume zao wanapotoka madarakani tu taasisi hizo hudhoofu na hazisikiki tena kwasababu waliokuwa wakipeleka misaada walikuwa wanalenga manufaa watakayoyapata,” alisema mtu mmoja ambaye hakutaja jina lake lichapishwe gazetini. 

"Ndiyo sababu si rahisi kwa sasa kusikia WAMA wala EOTF."
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Benson Bana alipinga hatua ya wake za marais kuanzisha asasi hizo akisema kuwa kwa nafasi zao zinawashushia heshima mbele ya jamii.
Alisema umefika wakati yaandikwe maadili ya wake za marais ili waepuke kuingia kwenye mitego kama hiyo ya kuanzisha asasi ambazo baadhi ya wachangiaji wake huzitumia vibaya.
“Maadili yasiishie kwa viongozi waliopigiwa kura tu hata wake za marais tunapaswa kuwawekea maadili maana sidhani kama ni mwafaka kwa mke wa rais kuanzisha taasisi," alisema Dk. Bana na kueleza zaidi:
"Tumeshuhudia asasi kama ya WAMA ikijikita zaidi Mkoa wa Pwani na kwao Lindi wakati yeye ni mama wa taifa.”
Aidha, Dk. Bana alisema hata kama mke wa Rais atakuwa alianzisha asasi hiyo kabla ya mume wake kuingia madarakani, anapaswa kuikabidhi kwa watu wengine waiendeshe na yeye ajikite kwenye masuala ya kitaifa.


“Mke wa Rais anapoanzisha asasi halafu anakwenda kuomba misaada inakuwa aibu na misaada yenyewe manufaa yake kwa jamii huwa hayaonekani.

"Mifano tunayo EOTF na WAMA ukiwauliza Watanzania wangapi walinufaika nazo utashangaa.”
Dk. Bana alishauri mke wa Rais Magufuli, Janeth asiingie kwenye mtego huo na kwamba kama anataka kutoa misaada mbalimbali anaweza kufanya hivyo bila hata kuwa na asasi kama ilivyokuwa kwa watangulizi wake.


Alisema mke wa Rais anaweza kutoa mchango wake kwa jamii kwa kushiriki mijumuiko ya kuchangia fedha kwa ajili ya miradi mbalimbali kama elimu, afya na kusaidia watu wasiojiweza, hatua ambayo haiwezi kulalamikiwa wala kuchafua taswira yake.
“Lazima tuwe na maadili ya wake za marais, kwamba anaweza kufanya hili lakini hapaswi kufanya hili, tusiache tu mambo yakaenda bila kuwa na misingi, mimi naamini mke wa Rais hapaswi kuanzisha taasisi.”

Mhadhiri mwingine wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Kitila Mkumbo alisema haoni ubaya wowote kwa mke wa Rais Magufuli kuanzisha taasisi ya kusaidia wananchi kama walivyofanya watangulizi wake.

Alisema duniani kote wake za marais wamekuwa wakianzisha taasisi kama hizo kwa ajili ya kusaidia wanawake wenzao, watoto na jamii kwa ujumla.

“Ukiwa mke wa rais unakuwa mama wa taifa na kuna mambo unapaswa kuyafanya kuonyesha kwamba wewe ni mama wa taifa, haitoshi kumuona tu mke wa Magufuli, Janeth akiambatana mumewe kwenye mikutano," alisema Profesa Mkumbo.

“Yeye ni mama wa taifa na mimi sitashangaa wala sitaona ubaya wowote nikisikia ameanzisha taasisi kama wenzake... hivyo namshauri aanzishe na kama akitaka washauri kwenye eneo hilo tupo.”

Nipashe ilifika katika ofisi zilizokuwa zikitumiwa na WAMA na kukuta kukiwa kimya huku walinzi ambao ni Polisi na kampuni binafsi wakiendelea na ulinzi wa maeneo hayo yaliyo ndani ya uzio wa Ikulu.

Mmoja wa walinzi hao ambaye alizungumza kwa sharti la kutojawa jina kwa sababu si msemaji, alisema mama Kikwete alishahamishia ofisi hiyo katika jengo la KFC, maeneo ya Mikocheni, jirani na nyumbani kwa hayati baba wa Taifa, Julius Nyerere.

Hata hivyo, alipoulizwa kama Mke wa Magufuli ameshaanzisha ofisi hapo, alisema hajaona dalili zozote.

Alisema kwa sasa hakuna shughuli yoyote inayoendelea kwenye jengo hilo na gazeti hili lilishuhudia hali ya utulivu eneo hilo huku milango ya jengo hilo ikiwa imefungwa.


Na Nipashe

No comments:

Post a Comment