Sunday 14 August 2016

Idadi ya waomba viwanja Dodoma yafikia hapa.

TANGU Rais John Magufuli atangaze uamuzi wa Serikali kuhamia Dodoma, kumekuwa na mwamko mkubwa wa wananchi kutoka maeneo mbalimbali nchini kutaka viwanja na hadi sasa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA) imepokea maombi 3,500 ya watu wanaotaka viwanja.

Aidha, wafanyabiashara katika masoko mbalimbali ya Dodoma wamesema hawana mpango wa kupandisha bei ya vyakula hata serikali itakapohamia rasmi, kwani vipo vingi na wamejipanga kuongeza mitaji ili kuendana na kasi ya ongezeko la watu.

Ofisa Uhusiano wa CDA, Angela Msimbira alisema mpaka sasa maombi yaliyopokelewa ni takribani 3,500 kwa ajili ya viwanja vya makazi na taasisi mbalimbali.

Alisema wizara karibu zote zimeshatuma maombi ya kupatiwa maeneo, mifuko ya hifadhi ya jamii, makanisa, shule, vyuo, Chama cha Walimu Tanzania (CWT) na watu binafsi.

“Wengi wanaoomba viwanja wanatoka maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Dar es Salaam na wamo pia watumishi wa serikali,” alisema Msimbira na kuongeza kuwa, wananchi na wakazi wa Dodoma nao wamehamasika kulipia viwanja. “Kuna watu walipatiwa viwanja na mamlaka tangu mwaka 2009 walikuwa kama wamevitelekeza, lakini sasa wanakuja kuvilipia,” alisema.

Alisema kwa sasa mapato ya mamlaka yanaongezeka kwa kuwa hata wasio na mazoea ya kulipia viwanja sasa wanavilipia.

“Mwamko umeongezeka kwa asilimia 100, kwa siku moja tunapokea wateja hadi 150 ambao wanafika kwenye mamlaka kwa ajili ya kulipia viwanja na kuchukua ‘bili’ (ankara) zao,” alisema Msimbira.

Pia alisema watu wengi sasa wanaulizia kama watapata nafasi ya kupanga katika nyumba za mamlaka wakiwemo watumishi wa serikali na watu binafsi.

Alisema mamlaka ina nyumba 583 zikiwemo 174 za ghorofa ambazo wapangaji wake waliondolewa kwa ajili ya kupisha ukarabati mkubwa unaotarajiwa kufanyika kuboresha nyumba hizo pamoja na mifumo yake. Hata hivyo, alisema baada ya ukarabati kumalizika watapangishwa watu watakaokidhi vigezo vitakavyotolewa na mamlaka.

Pamoja na hayo amewataka wananchi kote nchini wanaohitaji viwanja Dodoma kuvuta subira, kwani utaratibu wa kusanifu viwanja na kuvipima katika maeneo mbalimbali unaendelea. Amesisitiza wasinunue maeneo yasiyopimwa na CDA.

USISAHAU KULIKE NA KUSHARE PAGE YETU FACEBOOK TIKISA MEDIA KUFOLLOW TWITTER @TIKISA MEDIA NA INSTAGRAM TIKISA ENTERTAINMENT MEDIA ILI HABARI ZOTE KUBWA ZIKUFIKIE HAPA ULIPO.ASANTE

No comments:

Post a Comment