Wednesday 24 August 2016

Jaji Mutungi anena haya kuhusu Upepo wa siasa nchini, ikiwemo opesheni UKUTA ya CHADEMA.

MSAJILI wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi amewatoa hofu wananchi kuwa hakutakuwa na uvunjifu wa amani kutokana na sintofahamu inayoendelea nchini baina ya vyama vya siasa.


Alisema suala hilo litajadiliwa kwa njia ya busara na amani kwa kufanya mazungumzo na kamwe wananchi wasiaminishwe kuwa kuna ombwe la utendaji na kwamba hakuna njia ya suluhu katika masuala ya siasa.

Jaji Mutungi ambaye ni Mlezi wa Vyama vya Siasa nchini, amevisihi vyama vyote vyenye mipango ya kufanya mikutano au maandamano wasubiri yafanyike kwanza mazungumzo mapema wiki ijayo ili upatikane ufumbuzi unaostahili.

Aliwaambia waandishi wa habari jana Dar es Salaam kuwa Baraza la Vyama vya Siasa limeitisha mkutano maalumu kujadili changamoto na kuhakikisha wanamaliza sintofahamu iliyopo.

Alisema kikao hicho cha siku mbili kitatanguliwa na Kamati ya Uongozi itakayokaa na kupanga namna ya kufanya majadiliano hayo na kufikia muafaka.

Jaji Mutungi alisema kikao hicho kitafanyika Agosti 29 na 30, mwaka huu, na wamealika wageni mbalimbali kuzungumzia masuala hayo yaliyojitokeza na kuleta sintofahamu ili kuepuka nchi kuwa mfano wa kusema yalijitokeza haya kutokana na kutoelewana.

“Kwa kikao hiki cha baraza ambacho kitashirikisha wanachama wake kutoka vyama vyote vya siasa watafanyia kazi sintofahamu zilizojitokeza na kufikia muafaka hivyo wananchi hawatakiwi kuwa na hofu,” alisema Jaji Mutungi.

Hivi karibuni, kumeibuka taharuki miongoni mwa wananchi kuhusu Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kutangaza operesheni mpya iliyopewa jina la Umoja wa Kupambana na Udikteta Tanzania (Ukuta) ambayo itaanza kwa maandamano nchi nzima Septemba mosi, mwaka huu.

Kutokana na kutangaza operesheni hiyo itakayofanyika kwa kuandaa mikutano ya hadhara na maandamano, Rais John Magufuli aliingilia kati na kupiga marufuku kwa kuwaasa kutomjaribu kwa kufanya operesheni hiyo jambo lililoungwa mkono na Msajili huyo.

Lakini Chadema imeendelea kusisitiza kufanyika kwa maandamano na mikutano hiyo ambayo pia imepigwa marufuku na Jeshi la Polisi ambalo katika siku za karibuni limeonekana likifanya mazoezi ambayo wananchi wameyaelezea kuwa ni kupambana na watakaoshiriki katika operesheni hiyo.

Jaji Mutungi aliongeza kuwa yeye kama mshiriki atapata nafasi ya kuzungumzia mambo yaliyosababisha sintofahamu ikiwa ni pamoja kuzuiwa kwa shughuli za vyama vya siasa na nini Katiba inasema pamoja na changamoto nyingine kwa lengo la kutoa ufafanuzi.

USISAHAU KULIKE NA KUSHARE PAGE YETU FACEBOOK TIKISA MEDIA KUFOLLOW TWITTER @TIKISA MEDIA NA INSTAGRAM TIKISA ENTERTAINMENT MEDIA ILI HABARI ZOTE KUBWA ZIKUFIKIE HAPA ULIPO.ASANTE

No comments:

Post a Comment