Friday 5 August 2016

Serikali kudhibiti madereva wazembe barabarani kwa kutumia mfumo huu mpya.

SERIKALI imeanza rasmi kutumia mfumo wa nukta katika leseni za udereva kwa kudhibiti madereva wazembe, wanaosababisha ajali za barabarani.

Mfumo wa nukta ni mfumo ambao utatumika kupunguza nukta katika leseni za madereva, ambao watakutwa na makosa mbalimbali ikiwemo ulevi na uzembe, hatua ambayo baadaye itamfanya dereva kunyang’anywa leseni yake.

Hayo yalisemwa jijini Dar es Salaam jana na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Hamad Yusufu Masauni wakati wa uzinduzi wa Mkakati wa Kukabiliana na Ajali za Barabarani nchini.

Alisema mfumo huo, utakuwa na nukta 15 na dereva atakayebainika kutenda kosa la usalama barabarani, atapunguziwa nukta 10 kati ya 15 za leseni yake.

Alisema mkakati huo uliozinduliwa jana, ambao utadumu kwa kipindi cha miezi sita, umelenga kudhibiti makosa yanayosababisha madhara makubwa, likiwemo ongezeko la ajali za barabarani zinazowasababishia watu wasio na hatia vifo na ulemavu.

Aliongeza kuwa mambo yaliyolengwa katika mkakati huo ni pamoja na kudhibiti madereva walevi na ambao wanaendesha kwa uzembe.

Alisema dereva ambaye atakamatwa kwa sasa akiendesha kwa uzembe au ulevi, atapelekwa mahabusu kwa saa 24, ndipo atapelekwa mahakamani kwani wamegundua wapo madereva wanaoendesha kwa uzembe, wakiamini kuwa wakikamatwa watatozwa faini ambazo wanaweza kuzimudu.

Pia alisema mkakati huo, unalenga kudhibiti mwendo kasi kwa madereva na wamiliki wa magari na kuhakikisha kunakuwepo na madereva wawili kwa safari za masafa marefu.
“Hatuwezi kuendelea kuona ajali za barabarani zikiongezeka na kupoteza maisha ya watu ambao wengi ni tegemezi matokeo yake watoto wanabaki yatima, naamini dereva akibaki na nukta tano sijui atafanya nini na leseni yake,” alisema Masauni.


Masauni alieleza kuwa kwa mwaka 2013, Mkoa wa Kipolisi Kinondoni uliongoza kwa kuwa na ajali zipatazo 6,589 ukifuatiwa na Mkoa wa Kipolisi Ilala uliokuwa na ajali 3,464 wakati mikoa ya Simiyu na Tanga ilikuwa na ajali chache, ambapo Simiyu zilitokea ajali 67 na Tanga ajali 96.

Mwaka 2014 Kinondoni na Ilala ziliongoza tena, ambapo ajali 3,086 zilitokea Kinondoni na Ilala ajali 2,516. Mikoa iliyokuwa na ajali chache ni Simiyu ajali 55 na Kagera ajali 29.

Alisema kuwa mwaka 2015 Mkoa wa Kipolisi Ilala, uliongoza kwa kuwa na ajali nyingi za barabarani, ambapo ajali 2,516 zilitokea mkoani humo, ukifuatiwa na Temeke uliokuwa na ajali 1,420 wakati mikoa ya Rukwa na Arusha ilikuwa na ajali chache.

Alibainisha kuwa mfumo endelevu wa wazi uliopo wa kutoa takwimu hizo ni kupitia taarifa za mwaka za Jeshi la Polisi (Polisi Annual Report), ambapo kila Mtanzania anaweza kupata taarifa hizo za ajali.

USISAHAU KULIKE NA KUSHARE PAGE YETU FACEBOOK TIKISA MEDIA KUTU FOLLOW TWITTER @TIKISA MEDIA NA INSTAGRAM TIKISA ENTERTAINMENT MEDIA ILI HABARI ZOTE KUBWA ZIKUFIKIE HAPA ULIPO.ASANTE

No comments:

Post a Comment