Friday 19 August 2016

Waziri Mkuu Kassimu Majaliwa atoa agizo hili kuhusu wakuu wa shule na wanafunzi hewa nchini.

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amewaagiza wakuu wa wilaya na maofisa elimu nchini, wafanye ukaguzi katika shule ili kubaini wanafunzi hewa kwenye mpango wa elimu bure.

Katika hatua nyingine, serikali imesema itawavua madaraka wakuu wa shule ambao hawataki kubadilika na kuwatimua walimu wote wanaotumia dawa za kulevya ikiwemo bangi, wasio na sifa ya kufundisha na wenye vyeti bandia kwani wamekuwa chanzo cha kudorora kwa ufaulu katika shule kongwe nchini.
Aidha, imeanza kutoa Sh bilioni 21 kila mwezi kama ruzuku ya uendeshaji shule za msingi na sekondari na posho ya madaraka kwa ajili ya wakuu wa shule na walimu wakuu.
Kuhusu kufanyika kwa ukaguzi katika shule ili kubaini wanafunzi hewa kwenye mpango wa Elimu Bure, Waziri Mkuu alitoa agizo hilo jana alipokutana na watumishi na viongozi wa Manispaa ya Ilala katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini Dar es Salaam.
“Kila mwezi serikali inapeleka shule zaidi ya shilingi bilioni 18 kugharimia elimu bure na sasa tumeanza kuona udanganyifu katika sekta ya elimu kwa kuwa na wanafunzi hewa. Wakuu wa Wilaya na Maofisa Elimu nendeni mkafanye ukaguzi ili mpate takwimu sahihi. “Mkiona takwimu ziwachanganya ni lazima mtoke maofisini na kwenda katika shule zilizo kwenye mpango wa elimu bure mkafanye uhakiki wa idadi ya wanafunzi,” alionya.
Wakati huo huo, Waziri Mkuu alisema maamuzi yanayotolewa kwenye vikao vya madiwani, lazima yawe na tija na aliitaka halmashauri hiyo kuhakikisha fedha zinazokusanywa zinatumika kuboresha shughuli za maendeleo badala ya kujilipa posho.
“Lazima mjipange vizuri na kupunguza changamoto zinazoikabili wilaya yenu. Malipo yote ni lazima yawe yale yaliyoainishwa katika waraka na si vinginevyo. Mtu wa Ilala unadai nauli ya Sh 200,000, hivi unakuwa unatoka wapi hata mimi wa Lindi silipwi nauli hiyo,” Waziri Mkuu alihoji na kushangazwa.
Alisema ni lazima halmashauri zote nchini, zizingatie Sheria za Mamlaka ya Serikali za Mitaa na watendaji wake wajiulize kama mambo wanayoyafanya yana tija na wanawatendea haki watu wanaowatumikia.
Alisema Serikali inataka kuwa na watumishi wanaotambua nafasi zao na watakaofanya kazi kwa uadilifu, uaminifu pamoja na uwajibikaji mkubwa hivyo kila mtu ahakikishe anafanya kazi vizuri na yenye matokeo chanya.
“Kuna watu wanaona ukuu wa idara ndiyo kila kitu, hata yule anayekimbiza mafaili hathaminiwi, hili si jambo jema, ninyi wote ni kitu kimoja, ni watumishi wa Serikali, hivyo kila mmoja amthamini mwenzake,” alisema na kuongeza; “Mkurugenzi yeyote asikubali kuwa na wakuu wa idara wasiokuwa na ushirikiano na watumishi wengine kwa sababu hataweza kupata mafanikio ya kiutendaji ndani ya eneo lake.”

USISAHAU KULIKE NA KUSHARE PAGE YETU FACEBOOK TIKISA MEDIA KUFOLLOW TWITTER @TIKISA MEDIA NA INSTAGRAM TIKISA ENTERTAINMENT MEDIA ILI HABARI ZOTE KUBWA ZIKUFIKIE HAPA ULIPO.ASANTE

No comments:

Post a Comment