Monday 23 August 2021

Tetesi za Soka Ulaya Jumatatu 23.08.2021

Manchester City wanatarajia kupeleka ofa ya mwisho kwa ajili ya kumsaini mshambuliaji wa Tottenham Harry Kane wiki hii. Hatma ya nahodha huyo wa England, ambaye aliingia akitokea benchi kwenye mechi dhidi ya Wolves, haieleweki huku mwenyekiti wa Spurs Daniel Levy akitaka kumbakisha muingereza huyo mwenye umri wa miaka 28 (Telegraph)

Tottenham wanaangalia uwezekano wa kupeleka ofa ya £40m kwa ajili ya winga wa Wolves Adam Traore wakati huu ambapo kocha wa Spurs Nuno Espirito Santo akitaka kuungana na nyota huyo wa kimataifa wa Hispania, ambaye alimnoa pale Molineux kwa miaka mitatu. (Telegraph)

Manchester United imepata nguvu zaidi katika mbio zao za kumuwania mshambuliaji wa Borussia Dortmund Erling Braut Haaland, 21, ambaye kipengele cha mkataba wake kinachotaka dau la £64m ili kumuuza kitaanza kufanya kazi Januari. (Marca - in Spanish)

Tottenham bado wanamtaka kiungo wa Lyon na Ufaransa Houssem Aouar, 23, ambaye anatakiwa pia na Juventus. (Calciomercato - in Italian)

Arsenal ilishindwa kumsajili Manuel Locatelli, 23 kabla ya kiungo huyo wa Italia kujiunga na Juventus kwa mkataba wa mkopo wa miaka miwili, licha ya kutoa ofa kubwa ya pesa kwa Sassuolo kuliko magwiji hao wa Serie A , hiyo ni kwa mujibu wa mtendaji mkuu wa timu hiyo, Giovanni Carnevali. (Gazzetta di Modena - in Italian)

Tottenham wanamuwania kiungo mshambuliaji wa timu ya taifa chini ya miaka 21 ya England Noni Madueke, lakini PSV Eindhoven imewaambia wakali hao wa London kwamba itawagharimu dau la £40m ili kumsajili kinda huyo, ambaye aliondoka Spurs na kujiunga na klabu hiyo ya ligi ya Uholanzi ya Eredivisie mwaka 2018. (Mirror)

Spurs pia inataka kumsajili kiungo wa Senegal Pape Matar Sarr, 18, kutoka Metz huku rais wa klabu hiyo ya Ufaransa Bernard Serin akithibitisha kwamba wako kwenye mazungumzo ya mwisho mwisho na klabu ya ligi kuu England kuhusu uhamisho huo utakaogharimu zaidi ya £11m. (Le Republicain Lorrain - in French)

No comments:

Post a Comment