Tuesday 16 February 2016

Wasifu wa Yoweri Museveni

Rais Yoweri Museveni ameongoza Uganda kwa miaka 30, baada ya kuchukua uongozi akiwa kiongozi wa kundi la waasi.
Katiba, iliyokuwa imeweka kikomo kwenye muhula wa rais, ilifanyiwa marekebisho kumruhusu kuwania urais mwaka 2006 na baadaye akashinda tena uchaguzi februari 2011.
Katika uchaguzi wa 2011, alipata asilimia 68 ya kura dhidi ya mpinzani wake mkuu KizzaBesigye aliyepata asilimia 26. Besigye alipinga matokeo hayo akisema kulikuwa na udanganyifu.
Umoja wa Ulaya ulisema mfumo wa uchaguzi ulikuwa umeimarika ikilinganishwa na 2006, lakini bado kulikuwa na kasoro nyingi.
Bw Museveni amesifiwa kwa kuhakikisha uthabiti kisiasa pamoja na ukuaji wa uchumi Uganda baada ya miaka mingi ya vita vya wenyewe kwa wenyewe na ukandamizaji wa wapinzani chini ya watangulizi wake Milton Obote na Idi Amin.
Bw Museveni alikuwa mmoja wa waasisi wa kundi mojawapo la waasi waliosaidia wanajeshi wa Tanzania waliomuondoa mamlakani Idi Amin mwaka 1979. Baadaye aliunga jeshi ljipya la waasi ambalo lilifanikiwa kutwaa uongozi 1986.
Chama chake cha National Resistance Movement (NRM) kilitawala Uganda kama taifa la chama kimoja hadi pale kura ya maamuzi ilipofanyika 2005 na mfumo wa siasa za vyama vingi ukarejeshwa.
Alishinda uchaguzi wa urais 1996, 2001, 2006 na 2011.
Amekuwa akishutumiwa na Umoja wa Mataifa kwa mchango wake katika vita DR Congo kati ya 1998 na 2003. Majuzi zaidi, ametuhumiwa kuunga mkono makundi ya waasi huko.

Serikali yake pia imekuwa ikikosolewa kwa kutochukua hatua kali dhidi ya maafisa wakuu wanaodaiwa kujihusisha na ufisadi.
Kuna uvumi kwamba Bw Museveni anamtayarisha mwanawe Muhoozi Kainerugaba kuwa mrithi wake.
Aliyekuwa waziri mkuu Amama Mbabazi, aliyefutwa kazi 2015 katika hatua iliyoonekana kama ya kutaka kumuondoa mpinzani mtarajiwa wa Museveni, ni mmoja wa wanaowania urais uchaguzi wa Februari 2016.
Museveni alizaliwa magharibi mwa Uganda mwaka 1944, akasomea sayansi ya siasaTanzania na alipigana pamoja na wapiganaji wa Front for the Liberation of Mozambique (Frelimo), ambapo alipata ujuzi wa vita vya msituni.

No comments:

Post a Comment