MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imetangaza mwelekeo wa mvua
nchini katika kipindi cha mwaka huu na kusema mvua za masika huenda
zikaleta mafuriko na milipuko ya magonjwa hasa malaria.
Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk Agnes Kijazi alitoa taarifa hiyo ya
mwelekeo huo ikiwa tayari mvua za masika zimeanza kunyesha maeneo
mbalimbali nchini ikiwemo jijini Dar es Salaam.
“Mvua za Masika zinatarajiwa kuanza katika wiki ya kwanza na ya pili
ya mwezi Machi 2016 katika maeneo ya Ukanda wa Ziwa Viktoria na kusambaa
katika maeneo mengine yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka,”
alisema Dk Kijazi.
Aidha mvua hizo zinatarajiwa kuwa za wastani hadi juu ya wastani
katika maeneo mengi. Hata hivyo maeneo machache yanatarajiwa kupata mvua
za wastani hadi chini ya wastani. Mvua za msimu zinazoendelea
zinatarajiwa kunyesha katika kiwango cha wastani hadi chini ya wastani
katika maeneo mengi.
TMA ilieleza kuwa kunyesha kwa mvua hizo ni faraja kwa wafugaji,
kwani upatikanaji wa malisho unatarajiwa kuwa wa kuridhisha hususan
katika maeneo ya Ukanda wa Ziwa Viktoria na Nyanda za juu kaskazini
Mashariki.
Pia wakulima wa maeneo yote ambayo mvua hizo zitanyesha zitasaidia
kuwepo kwa hali ya unyevunyevu wa udongo na kuwa ya kutosheleza shughuli
za kilimo katika maeneo mengi. Hata hivyo, mvua za juu ya wastani
zinazotarajiwa kunyesha zinaweza kusababisha hali ya unyevunyevu wa
udongo kupita kiasi hivyo kuathiri mazao.
TMA pia ilisema mlipuko wa magonjwa kama vile Malaria unatarajiwa
kujitokeza baada ya kunyesha kwa mvua hizo huku vipindi vya mvua kubwa
vinaweza kusababisha mafuriko. Mamlaka za miji nchini zimetakiwa
kuchukua tahadhari, ikiwa ni pamoja na kuimarisha mifumo ya maji taka
huku mamlaka za afya zikitakiwa kuchukua tahadhari dhidi ya milipuko ya
magonjwa.
Wednesday 9 March 2016
TMA imetangaza hali ya hatari juu ya mvua zinazoendelea kunyesha nchini
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment