Sunday 17 July 2016

Baraza la Vijana Chadema kurudi tena Dodoma tarehe 20 kwa hoja hii.

BARAZA la Vijana wa Chadema (Bavicha) limepanga kufanya mkutano wa Kamati ya Utendaji ya baraza hilo Julai 20, mwaka huu mkoani Dodoma ambao utatoa mwelekeo wa kupigania demokrasia.

Aidha, limewataka vijana wa chama hicho nchi nzima kuwa watulivu na kutii agizo la Mwenyekiti wa chama hicho taifa, Freeman Mbowe wakati wakisubiri maamuzi ya kikao hicho.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Bavicha Taifa, Patrobas Katambi alisema, baraza hilo linaona kama jeshi la polisi halitendi haki kwa kuruhusu mkutano wa CCM, jambo alilosema ni ukandamizaji wa demokrasia.

“Kikao chetu cha Kamati ya Utendaji tulikuwa tumekiahirisha baada ya polisi kuzuia, lakini sasa tunafanya tena kwa tarehe ileile ambayo ni Julai 20 mjini Dodoma ambapo tulipanga kufanya mwanzo,” alisema.

Aidha, Katambi alisema Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP), Ernest Mangu hana budi kujiuzulu iwapo mkutano huo wa CCM utafanyika kwa kuwa atakuwa ameshindwa kusimamia kauli ya jeshi hilo lakini pia ya Rais John Magufuli.

Alisema baada ya Mbowe kuwazuia wasiende Dodoma wameamua kuja na mpango wa pili ambapo hawatakwenda Dodoma lakini hawataruhusu mkutano wa CCM ufanyike hadi serikali itakapotoa kauli ya haki sawa za kidemokrasia kwa kila chama.

Katibu Mkuu wa baraza hilo, Julius Mwita alisema, hawaoni kama kufanyika kwa mkutano wa kamati ya utendaji kutaathiri kwa namna yoyote usalama wa wanachama au mkutano wa CCM.

Alisema tayari hata IGP anajua kuwa watafanya mkutano wao mjini Dodoma lakini watampa taarifa ukumbi utakaofanyika mkutano huo baada ya kuupata na kukubaliana na mwenye ukumbi.

No comments:

Post a Comment