Monday 1 August 2016

Rais Magufuli atoa Tamko hili kuhusu Bodi ya pamba Tanzania(TCB).

RAIS John Magufuli ameiagiza Bodi ya Pamba Tanzania (TCB) kuhamia katika mikoa ya Kanda ya Ziwa na kuondoka Dar es Salaam, kwa sababu huko ndiko ambako wakulima wengi wa zao hilo wanapatikana.


Aidha, ameionya bodi hiyo kwamba hataki kusikia kwamba imetoa tena mbegu zisizoota kwa wakulima, na endapo hilo litatokea, atawatumbua viongozi wake.

Rais Magufuli aliyasema hayo mjini Geita wakati akizungumza na wananchi, akiendelea na ziara zake katika mikoa ya Singida, Tabora, Shinyanga na Geita, ambayo aliianza mwishoni mwa wiki iliyopita.

Alisema inashangaza kuona kuwa Bodi ya Pamba iko Dar es Salaam wakati wakulima wengi wa zao la pamba wanapatikana katika mikoa ya Kanda ya Ziwa ya Geita, Mwanza, Shinyanga, Mara, Simiyu na Kagera, hivyo kuwataka wahamie katika mikoa hiyo na kuwa karibu na wakulima hao.

Akiwa Isaka, Rais Magufuli alisema hatalipa fidia kwa nyumba takribani 300 kwa sasa, badala yake kazi kubwa atakayoifanya ni kuhakikisha anamaliza tatizo la maji katika mji huo, ambalo linawasumbua wananchi kwa muda mrefu. Imeandikwa na Raymond Mihayo na Kareny Masasi.

No comments:

Post a Comment