Thursday 31 August 2017

Rais wa TFF Wallace Karia aanza kuwasha moto atoa maagizo mazito.

Image result for Wallace Karia
Rais wa TFF Wallace Karia ameagiza bodi ya ligi kuwachukulia hatua watendaji wote wa bodi hiyo waliyoharibu kwenye upangaji wa ratiba ya michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara ambayo kwa sasa imesogezwa mbele.


Karia ametoa agizo hilo kufuatia malalamiko ya wadau kuhusu mabadiliko yaliyofanywa kwenye ratiba hiyo ikiwemo kusogezwa mbele kwa michezo ya raundi ya pili ya ligi ambayo sasa imepangwa kupigwa Septemba 6, 2017 badala ya Septemba 2 iliyokuwa imepangwa awali, kwa madai ya kupisha mechi ya Taifa Stars dhidi ya Botswana iliyo kwenye kalenda ya FIFA.

Rais huyo ambaye awali alikuwa ndiye Makamu na Kaimu Rais kabla ya kuingia rasmi madarakani kupitia uchaguzi mkuu uliofanyika Agosti 12 mwaka huu, amesema kabla ratiba hiyo haijatoka, alitoa maagizo kwa bodi hiyo kuzingatia kalenda ya FIFA katika upangaji wake, lakini ameshangaa kuona agizo hilo kutozingatiwa.

Akizungumza na chombo kimoja cha habari, Karia amesema kuwa siku alipochaguliwa aliahidi kuchapa kazi na watu makini, na kwamba aliahidi kuwa, katika kipindi chake “wababaishaji hawatakuwa na nafasi”, hivyo ni lazima achukue hatua kwa yeyote anayeonekana kukwamisha maendeleo ya soka au kuchafua taswira ya shirikisho hilo.

Mbali na suala la ratiba, Karia amesema pia kuwa sakata la makosa ya maandishi kwenye ngao ya jamii iliyokabidhiwa kwa Simba Agosti 23, mwaka huu, halijamuacha mtu salama, kwani wote waliohusika na makosa yale, tayari wamewajibishwa.

No comments:

Post a Comment