Monday 6 May 2019

Hivi ndivyo linavyoandaliwa kaburi la Dkt. Reginald Mengi,


MAANDALIZI ya kaburi atakamopumzishwa aliyekuwa Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP, Dkt. Reginald Mengi, yanaendelea nyumbani kwao katika Kijiji cha Nkuu Sinde, Machame Mashariki mkoani Kilimanjaro ambapo vijana wameendelea kuchimba kaburi hilo lililopo eneo ambalo walizikwa wazazi wake pamoja na mwanaye Rodney Mengi aliyefariki dunia mwaka 2005.



Dkt Mengi ambaye alikuwa mfanyabiashara maarufu ndani na nje ya nchi alifariki dunia Mei 2, 2019, Dubai na mwili wake utawasili nchini leo Mei 6, 2019, saa 8:00 mchana kwa ndege ya shirika la Emirates.

Kesho Jumanne, utaagwa Dar es Salaam na Jumatano utasafirishwa kwenda Machame kwa maziko yatakayofanyika Alhamisi.



Baada ya mwili kupokelewa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, utapitishwa maeneo ya Tazara, Buguruni, Ilala, Kigogo, Magomeni, Kinondoni, Morocco, Barabara ya Bagamoyo, Sayansi, Mwenge hadi katika Hospitali ya Jeshi Lugalo ambako utahifadhiwa.

Ratiba hiyo itaendelea siku ya Jumanne ya Mei 7, 2019, ambapo mwili utapelekwa katika ukumbi wa Karimjee, kwa ajili ya watu  kuuaga na kisha utarejeshwa nyumbani kwake. Siku ya Jumatano mwili utasafirishwa kupelekwa Moshi Machame ambako ibada ya mazishi itafanyika siku ya Alhamisi katika kanisa la KKKT Kisereni

No comments:

Post a Comment