Tuesday 7 April 2020

Maharusi wamekamatwa Afrika Kusini kwa kufunga ndoa.

Wanandoa wapya wajipata matatani huko Afrika Kusini punde tu baada ya kufunga pingu za maisha. 


Maharusi hao walivamiwa na maafisa wa polisi baada ya kudokezewa kwamba kuna harusi inayoendelea huko KwaZulu-Natal licha ya marufuku ya kukusanyika kwasababu ya virusi vya corona. 

Wageni 50 waalikwa na kasisi aliyewafunganisha pamoja na wanandoa wenyewe walikamatwa na maafisa wa polisi na kupelekwa katika kituo cha polisi nje ya mji wa Richards Bay.

Kundi lote hilo lilifikishwa mahakamani.
Video iliyosambaa mtandaoni inamuonesha bwana harusi akimsaidia bibi harusi kwa kushika gauni lake jeupe wakati wanaingia kwenye gari la polis
Majina ya wanandoa hao wapya hayakuwekwa hadharani na maafisa wa polisi wala vyombo vya eneo. 

Aidha, manispaa ya Umhlathuze imesema kuwa maharusi hao watafurahia fungate yao chini ya dhamana kwa masharti watakayopewa.
Afrika Kusini ambayo imethibitisha visa 1,655 vya coronavirus, ikiwemo vifo 11, kwasasa iko katika wiki ya pili yenye masharti magumu kabisa ya 'lockdown' kama ilivyo kwa baadhi ya nchi duniani.
Pia imekuwa miongoni mwa nchi zenye kupima watu kutoka eneo moja hadi jingine na hivi karibuni itafikia uwezo wa kupima watu 30,000 kila siku. 

Raia Afrika Kusini wanaruhusiwa kutembea tu iwapo kuna ulazima wa kufanya hivyo na kama haitoshi pia kuna marufuku ya kununua pombe na sigara.
Wachambuzi wamekuwa wakikosoa jinsi nchi hiyo inavyokabiliana na janga la corona na shughuli zote nchini humo zimesitishwa ikiwa kwa 'lockdown' kwa kipindi cha wiki tatu za kwanza.

No comments:

Post a Comment