Wednesday 11 May 2016

Hapa kazi Tu ya Rais Magufuli baadhi ya watumishi wa serikali waanza kujiuzulu.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa George Simbachawene amesema kasi ya Rais Dkt John Magufuli na serikali yake tayari watumishi wameanza kuandika barua za kuomba kujiuzulu na kutafuta kazi sehemu nyingine.

Waziri Simbachawene ameyasema hayo ingawa hajataja majina ya watumishi hao na halmashauri wanazotoka, katika kipindi cha dakika 45 kinachorushwa na ITV na kusema kuwa yeye binafsi ameshapokea barua za watumishi watatu kutoka kwenye halmashauri ambao hawana makosa yoyote ya kiutendaji lakini wameamua kuandika barua ya kuomba kuachia kazi hizo.

''Kasi ya Rais Dkt. Magufuli haitawaacha watumishi wazembe wameendelee kufanya kazi kwa maana mazoea kazini hayapo ndiyo maana mimi nimeshapokea barua ya watumishi watatu wakiomba kujiuzulu nyazifa zao na kweli kama kuna kiongozi anaona hataweza kwenda na kasi ya Rais na Wizara yangu ni bora aondoke mapema kabla sijatumbuliwa mimi nitawatumbua wao''. Amesisitiza Chawene.

Aidha Waziri Simbachawene ameeleza kusikitishwa kwake na watumishi ambao wameshindwa kuwapandisha madaraja watumishi waliopo chini yao kwa uzembe wao jambo ambalo linawafanya watumishi kuishi kwa malalamiko na kukosa imani na serikali yao.

''Mimi sitamvumilia afisa utumishi yeyote ambaye hatawapandisha madaraja watumishi waliopo chini yake wakati sifa wanazo huko ni kuharibu maisha ya watu na serikali hii haipo tayari kuvumilia watumishi kama hao'' Amesema Waziri Simbachawene.

No comments:

Post a Comment