Tuesday 17 May 2016

Kauli ya mama Anna Mghwira kuhusu utumbuaji majipu wa Rais Dk.Magufuli.

 
Mwenyekiti wa ACT Wazalendo Mama Anna Mghwira amesema kitendo cha serikali ya awamu ya tano kutumbua majipu
kinawafanya wananchi kuhamishwa kwenye mambo ya msingi na kujikita kwenye jambo moja la utumbuaji majipu.

Mama Mghwira ameyasema hayo na kusisitiza   kwamba wananchi wengi kwa sasa wanatizama taarifa za habari wakitaka kujua ni nani ambaye ametumbuliwa na hii inaonyesha dhahiri kwamba wananchi walikuwa wamechoshwa na suala la utumishi mbofu pamoja na rushwa iliyokithiri serikalini.

''Kuna mambo mengi yanahitaji mijadala ya msingi lakini watanzania ni wepesi sana kuhamishwa hamishwa kwenye mambo ya msingi mfano suala la katiba mpya, mfumo wa elimu, kutorushwa bunge live, Lugumi, sakata la sukari, ni baadhi ya mambo ambayo watu walitakiwa wajikite hasa na kupata majawabu ya msingi''.Ameeleza Mghwira.

''Wananchi wanafurahia lakini kwa mtizamo wangu hapati majawabu sahihi ya wanaotumbuliwa kwa mfano utumbuaji uliofanyika bandarini mwendelezo wake upo wapi au ni maendeleo gani yamepatikana kufuatia utumbuaji huo wa majipu na waliofanya hivyo wapo wapi''- Amesisitiza Mghwira.

Aidha Mama Mghwira amesisitiza uwepo wa katiba mpya nchini na kusema kuwa kama yeye angekuwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania angerejesha kumaliziwa kwa katiba mpya ya wananchi ili kuweza kutumia katiba itakayokuwa inatoa muongozo sahihi katika vitu muhimu vya nchi.

No comments:

Post a Comment