Thursday 10 August 2017

Mbaraka Yusuph wa Azamu FC atamba kuchukua Kiatu cha Dhahabu msimu ujao Ligi kuu.


Image result for Mbaraka Yusuph
Wakati msimu wa 2017/18 ukielekea kuanza, tayari majigambo yameanza kuwa mengi, kuhusu  mfungaji bora katika msimu ujao ambao unatarajiwa kuwa na ushindani mkali.


Mshambuliaji mpya wa Azam FC, Mbaraka Yusuph, ameahidi kuibuka mfungaji bora wa michuano ya Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) inayotarajia kuanza Agosti 26 mwaka huu.

Yusuph aliyesaini mkataba wa miaka miwili ni miongoni mwa washambuliaji wapya waliosajiliwa kwa ajili ya msimu ujao akitokea Kagera Sugar alikofunga mabao 12 msimu uliopita na kuchaguliwa kuwa Mchezaji Bora Chipukizi.

Kauli hiyo ni kama dongo zito kwa wachezaji wengine hasa wa Simba na Yanga ambao wanatajwa kuwa wanaweza kuwa na nguvu katika kupigania kiatu cha dhahabu cha ufungaji bora kwa ajili ya msimu ujao. Baadhi ya wachezaji hao ni Amiss Tambwe wa Yanga, Emmanuel Okwi na Shiza Kichuya wa Simba.. 

“Kwa kweli nimejipanga kufanya vizuri zaidi kuliko msimu uliopita, natarajia Mwenyezi Mungu akinijalia kila mechi nitakayocheza niweze kupata nafasi, niweze kufunga na kuwa mfungaji bora wa ligi,” alisema Yusuph.

Yusuph ambaye ni shabiki mkubwa wa staa wa Baracelona na Argentina, Lionel Messi, amewapa ahadi mashabiki wa Azam FC ya timu hiyo kufanya vizuri msimu ujao huku akiwaomba waisapoti zaidi timu hiyo.

No comments:

Post a Comment