Thursday 10 August 2017

Timbulo aweka wazi ukweli kuhusu Mo-Music.


Msanii Timbulo amesema ameshangazwa na tuhuma zinazotolewa na msanii mwenzake Mo Music kuwa anambania kurudi kwenye uongozi wake wa awali, kitu ambacho hakina ukweli wowote.

Akizungumza kwenye kipindi cha eNewz kinachorushwa na East Africa Television, Timbulo amesema yeye ni miongoni mwa watu ambao walikuwa mstari wa mbele kumsaidia Mo Music na hakutaka kutangaza juu ya hilo, hivyo anashangzwa na taarifa za kusema kuwa anambania.

“Mo music ni kijana ambaye natamani kumuona mbali zaidi kuliko alipo sasa  na bado naamini kuwa yeye ni msanii mzuri. Kuna siku atakaa vizuri na atarudi,  mimi nimemsaidia kwa kiwango kile ambacho niliweza na sikuwahi kusema popote kuhusu hilo, sisi kwa imani yetu tunaambiwa toa mkono wa kulia wa kushoto usijue ulichotoa kwa hiyo sikutaka kusema na hata sitakuja kusema", alisema Timbulo.

Timbulo aliendelea kusema kuwa hata Mo Music alipotaka kuondoka kwenye uongozi wao alimsihi asiondoke, lakini hakutaka kusikia na kuondoka.

“Mimi ni mmoja wa watu ambao wakati Mo Music anajaribu kutoka  kwenye management nilijaribu sana kumsisitiza na kumkataza asitoke, hata ilipofikia hatua kwamba lazima aondoke kwa maelezo yake nilijaribu kumsihi  asipige kelele kuhusiana na 'management' iliyopita kwa sababu hajui anakoenda, maneno ya hekima sana, baadaye yakabadilika na kuwa mengine", alisisitiza Timbulo.

Kwa upande mwingine, Timbulo amemtaka Mo Music ajitokeze katika vyombo vya habari na aseme amebaniwa kwa upande upi na kivipi.

No comments:

Post a Comment