Wednesday 14 February 2018

Mwisho wa Donald Ngoma Yanga kujulikana Ijumaa

Image result for Donald Ngoma
Uongozi wa klabu ya Yanga umefunguka kuwa hadi kufikia Ijumaa hii kila kitu juu ya hatma ya mshambuliaji wao, Donald Ngoma raia wa Zimbabwe kitakuwa kimejulikana.

Haya yametokea baada ya viongozi kukutana na kujadili ripoti ambayo waliomba waletewe na daktari wa timu hiyo juu ya ugonjwa wa mshambuliaji huyo.

Ngoma ameshindwa kuitumikia timu hiyo inayonolewa na kocha George Lwandamina raia wa Zambia kutokana na kuwa nje akiendelea kujiuguza majeraha ambapo kwa nyakati tofauti alikuwa anaumwa nyonga na goti.

Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Yanga, Hussein Nyika amesema kuwa hadi kufikia Ijumaa hii tayari watakuwa wameshajua hatma ya mshambuliaji huyo.

“Hili suala la majeraha ya mshambuliaji wetu Donald Ngoma hadi Ijumaa hii tutakuwa tumelipatia ufumbuzi baada ya kuipitia ripoti ambayo tuliiomba kutoka kwa daktari wetu baada ya kuona kwamba anaendelea kukaa nje bila ya kucheza.


“Ripoti tuliipata tangu wiki iliyopita lakini hatukuifanyia kazi kwa sababu mawazo yetu yalikuwa kwenye mchezo na St Louis na ule dhidi ya Majimaji (leo Jumatano), baadaye  nadhani tutatumia muda uliobakia kuipitia na hadi Ijumaa basi kila kitu kitakuwa kimejulikana,” alisema mwenyekiti huyo. 

No comments:

Post a Comment